Agano la Kale

Agano Jipya

Hesabu 31:21-38 Biblia Habari Njema (BHN)

21. Kuhani Eleazari akawaambia wanaume waliorudi vitani, “Hii ndiyo sheria ambayo Mwenyezi-Mungu amempa Mose.

22. Dhahabu, fedha, shaba, chuma, bati na madini ya risasi,

23. yaani vitu vyote ambavyo vinastahimili moto, vitatakaswa kwa kupitishwa motoni. Hata hivyo, ni lazima vitakaswe kwa maji ya utakaso. Vitu vingine vyote ambavyo haviwezi kustahimili moto vitatakaswa kwa maji ya utakaso.

24. Siku ya saba ni lazima muyafue mavazi yenu; ndipo mtakapokuwa safi na kuruhusiwa kuingia kambini.”

25. Mwenyezi-Mungu akaongea na Mose, akamwambia,

26. “Wewe na kuhani Eleazari, pamoja na viongozi wa koo za jumuiya ya Waisraeli, fanyeni hesabu ya nyara ya vitu, watu na wanyama.

27. Gaweni nyara katika mafungu mawili, fungu moja la wanajeshi waliokwenda vitani na fungu lingine kwa ajili ya jumuiya nzima.

28. Kisha kutokana na lile fungu la wanajeshi waliokwenda vitani, tenga zaka kwa ajili ya Mwenyezi-Mungu: Kitu kimoja kutoka kila vitu 500, iwe ni watu, ng'ombe, punda, kondoo au mbuzi,

29. umpe kuhani Eleazari kuwa sadaka kwa Mwenyezi-Mungu.

30. Kutoka lile fungu la jumuiya nzima, chukua sehemu moja ya kila hamsini, iwe ni watu, ng'ombe, punda, kondoo na mbuzi. Hivyo utawapa Walawi ambao wana wajibu wa kuhudumu katika hema la Mwenyezi-Mungu.”

31. Mose na kuhani Eleazari walifanya kama Mwenyezi-Mungu alivyomwamuru Mose.

32. Nyara walizoteka wanajeshi zilikuwa: Kondoo 675,000,

33. ng'ombe 72,000,

34. punda 61,000,

35. na wasichana ambao hawakuwa wamelala na mwanamume 32,000.

36. Nusu yake, sehemu ambayo iligawiwa wanajeshi waliokwenda vitani, ilikuwa kondoo 337,500,

37. katika hao 675 walitolewa kwa Mwenyezi-Mungu.

38. Ngombe wa wanajeshi walikuwa 36,000, na katika hao 72 walitolewa zaka kwa Mwenyezi-Mungu.

Kusoma sura kamili Hesabu 31