Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 38:13-23 Biblia Habari Njema (BHN)

13. Wakazi wa Sheba na Dedani pamoja na wafanyabiashara wa Tarshishi na vitongoji vyake watakuuliza, ‘Je, umekuja kuteka nyara? Je, umekusanya jeshi lako ili kushambulia na kutwaa nyara na kuchukua fedha na dhahabu, mifugo na bidhaa, na kuondoka na nyara nyingi?’

14. “Kwa hiyo, ewe mtu, toa unabii na kumwambia Gogu kwamba mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Wakati taifa langu la Israeli linaishi kwa usalama, wewe utafunga safari

15. kutoka kwenye maskani yako, huko mbali kabisa kaskazini, uje pamoja na watu wengi wakiwa wote wamepanda farasi: Jeshi kubwa na lenye nguvu.

16. Utawakabili Waisraeli, kama wingu linalotanda juu ya nchi. Wakati huo nitakutuma uishambulie nchi yangu, ili mataifa yajue kwamba nimekutumia wewe Gogu ili nioneshe utakatifu wangu mbele yao.

17. “Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema kwamba, wewe ndiwe niliyesema habari zako hapo kale kwa njia ya watumishi wangu manabii wa Israeli, ambao walitabiri nyakati zile kuwa baadaye nitakuleta upambane na watu wa Israeli.”

18. Bwana Mwenyezi-Mungu asema hivi: “Siku ile Gogu atakapoishambulia nchi ya Israeli, nitawasha ghadhabu yangu.

19. Mimi natamka rasmi kwa wivu na ghadhabu yangu kali kwamba siku hiyo kutakuwa na tetemeko kubwa la ardhi nchini Israeli.

20. Samaki baharini na ndege warukao, wanyama wa porini, viumbe vyote vitambaavyo pamoja na watu wote duniani, watatetemeka kwa kuniona. Milima itaporomoshwa, magenge yataanguka na kuta zote zitaanguka chini.

21. Nami nitasababisha kila namna ya tisho kumkabili Gogu. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema. Wanajeshi wake wataanza kushambuliana wenyewe kwa mapanga yao.

22. Nitamwadhibu Gogu kwa magonjwa mabaya na mauaji. Nitanyesha mvua nyingi, mvua ya mawe na moto wa madini ya kiberiti juu yake, juu ya vikosi vyake, na mataifa yale mengi yaliyo pamoja naye.

23. Ndivyo nitakavyofanya mataifa yote yaone ukuu wangu na utakatifu wangu. Ndipo watakapotambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu.”

Kusoma sura kamili Ezekieli 38