Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 36:3-23 Biblia Habari Njema (BHN)

3. “Kwa hiyo, wewe Ezekieli, toa unabii useme kuwa mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Watu wamewafanya nyinyi milima ya Israeli kuwa tupu na kuwavamia kutoka kila upande hata mmekuwa mali ya mataifa mengine, mkawa kitu cha kusimangwa na kudhihakiwa miongoni mwa watu!

4. Kwa hiyo, enyi milima ya Israeli, sikieni neno langu mimi Bwana Mwenyezi-Mungu: Nyinyi milima na vilima, mifereji na mabonde, nyika tupu na miji mmehamwa, mkatekwa nyara na kudharauliwa na mataifa yote yanayowazungukeni.

5. Sasa kwa kuwa mimi nimechukizwa mno, nitayaadhibu mataifa mengine na hasa watu wa Edomu. Wao kwa furaha moyoni na madharau waliichukua hiyo nchi iliyo yangu iwe yao.

6. Kwa hiyo, ewe mtu, toa unabii kuhusu nchi ya Israeli, uiambie milima na vilima, vijito na mabonde kuwa mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema mambo haya kutokana na ghadhabu yangu yenye wivu juu ya nchi yangu, kwa sababu imetukanwa na watu wa mataifa.

7. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Ninaapa kwamba watu wa mataifa yaliyo jirani nanyi watatukanwa wao wenyewe.

8. “Lakini kuhusu milima ya Israeli, miti itatoa matawi na kuzaa matunda kwa ajili ya watu wangu wa Israeli, maana wao watarudi makwao karibuni.

9. Mimi niko upande wenu, nitahakikisha kuwa mnalimwa na kupandwa mbegu.

10. Waisraeli nitawazidisha sana. Miji itakaliwa, na magofu yatajengwa upya.

11. Nitawafanya watu na wanyama waongezeke na kuwa wengi. Nitawafanya nyinyi milima mkaliwe tena kama zamani. Nitawatendea mema mengi kuliko zamani. Nanyi mtatambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu.

12. Nitawafanya watu wangu Israeli watembee juu yenu. Nanyi mtakuwa milki yao, wala hamtawafanya tena wafiwe na watoto wao.

13. “Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Kwa vile watu wamesema juu yenu kwamba mnakula watu, na mmelipokonya taifa lenu watoto wake,

14. basi, sasa hamtakula tena watu wala kupokonya taifa lenu watoto wake. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema.

15. Sitaruhusu tena mataifa yawatukane, wala kuwadharau tena. Hamtasababisha taifa lenu likose. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema.”

16. Neno la Mwenyezi-Mungu lilinijia:

17. “Wewe mtu! Waisraeli walipoishi katika nchi yao waliitia unajisi kwa mienendo na matendo yao. Niliyaona matendo yao kuwa sawa na mwanamke aliye najisi wakati wa siku zake.

18. Niliwamwagia ghadhabu yangu kwa sababu ya damu waliyomwaga katika nchi na kwa sababu ya miungu ambayo kwayo nchi ilitiwa unajisi.

19. Niliwatawanya kati ya mataifa, wakasambazwa katika nchi nyingine. Niliwaadhibu kadiri ya tabia yao na matendo yao.

20. Hata walipokuwa miongoni mwa mataifa walilikufuru jina langu takatifu, hata watu wakasema hivi juu yao: ‘Tazama! Hawa ndio wale watu wa Mwenyezi-Mungu, lakini wamelazimika kuondoka katika nchi yake!’

21. Hiyo ilinifanya kuhangaika juu ya jina langu takatifu ambalo watu wa Israeli walilikufuru miongoni mwa mataifa walikokwenda.

22. Basi, waambie Waisraeli kwamba mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Ninachotaka kufanya si kwa faida yenu nyinyi watu wa Israeli, bali ni kwa heshima ya jina langu takatifu mlilolikufuru miongoni mwa mataifa mlikokwenda.

23. Nitalirudishia hadhi yake takatifu jina langu kuu mlilokufuru miongoni mwa mataifa. Hapo ndipo mataifa yatakapotambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema. Nitawatumia nyinyi kuonesha utakatifu wangu mbele yao.

Kusoma sura kamili Ezekieli 36