Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 3:3-12 Biblia Habari Njema (BHN)

3. Halafu akaniambia, “Wewe mtu, kula kitabu hiki ninachokupa, ujaze tumbo lako.” Basi, nilikula kitabu hicho, nacho kikawa kitamu mdomoni kama asali.

4. Kisha akaniambia, “Wewe mtu, waendee Waisraeli, ukawaambie maneno yangu.

5. Sikutumi kwa taifa lenye lugha ngeni na ngumu, bali kwa Waisraeli.

6. Sikutumi kwa mataifa mengi yenye lugha ngeni na ngumu ambayo huifahamu. Kwani ningelikutuma kwa watu kama hao, hakika wao wangekusikiliza.

7. Lakini Waisraeli hawatakusikiliza, kwani hawana nia ya kunisikiliza mimi. Watu wote wa Israeli ni wenye kichwa kigumu na moyo mkaidi.

8. Nimekufanya uwe mgumu dhidi yao, na kichwa chako kitakuwa kigumu dhidi ya vichwa vyao vigumu.

9. Kama almasi ilivyo ngumu kuliko jiwe gumu, ndivyo nilivyokufanya uwe kichwa kigumu. Usiwaogope wala usitishwe na nyuso zao, kwani hao ni watu waasi.”

10. Tena aliniambia, “Wewe mtu, maneno yote nitakayokuambia yatie moyoni mwako, na uyasikilize kwa makini.

11. Kisha nenda kwa watu wako waliopelekwa uhamishoni, ukawaambie kwamba mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi na hivi. Waambie hata kama watakusikiliza au watakataa kukusikiliza.”

12. Kisha roho ya Mungu ikaninyanyua, nami nikasikia nyuma yangu sauti kama ya tetemeko kubwa. “Na usifiwe utukufu wa Mwenyezi-Mungu mbinguni.”

Kusoma sura kamili Ezekieli 3