Agano la Kale

Agano Jipya

Danieli 8:10-18 Biblia Habari Njema (BHN)

10. Upembe huo ulikua sana kufikia viumbe vya mbinguni; ukaziangusha chini baadhi ya nyota na kuzikanyagakanyaga.

11. Upembe huo ukajikweza juu ya mkuu wa viumbe vya mbinguni. Ukakomesha tambiko za kuteketezwa ambazo mkuu wa viumbe vya mbinguni alitambikiwa kila siku, na kukufuru maskani yake.

12. Viumbe vya mbinguni vikatiwa nguvuni mwake pamoja na tambiko za kuteketezwa kila siku, kwa njia ya upotovu. Nao ukweli ukatupwa chini. Upembe huo ukaibwaga chini ibada ya kweli. Ulifanikiwa katika kila jambo ulilofanya.

13. “Kisha, nikamsikia mtakatifu mmoja akizungumza na mwenzake. Huyo mwenzake alimwuliza, ‘Je, matukio yaliyotangazwa na maono haya yataendelea kwa muda gani? Kwa muda gani sadaka za kuteketezwa za kila siku zitabaki zimebatilishwa? Kwa muda gani upotovu wa kuangamiza kila kitu utaendelea, na mahali patakatifu pamoja na viumbe vya mbingu vitaendelea kukanyagwa?’

14. Yule mtakatifu wa kwanza akamjibu, ‘Kwa muda wa nyakati za jioni na asubuhi 2,300. Kisha maskani ya Mungu itapata tena hali yake halisi.’

15. “Mimi Danieli nilipoyaona hayo maono, na nilipokuwa nikijaribu kujua maana yake, ghafla, mmoja kama mwanaadamu akasimama mbele yangu.

16. Nikasikia sauti ya mwanaadamu kutoka katika mto Ulai ikiita, ‘Gabrieli, mweleze mtu huyu maana ya maono aliyoona.’

17. Gabrieli akaja karibu na mahali niliposimama. Mimi nikaogopa sana, hata nikaanguka kifudifudi. Lakini akaniambia, ‘Wewe mtu, elewa kwamba maono uliyoyaona yanahusu wakati wa mwisho.’

18. “Alipokuwa anazungumza nami, mimi nikashikwa na usingizi mzito huku nimelala kifudifudi. Lakini yeye akanishika na kunisimamisha.

Kusoma sura kamili Danieli 8