Agano la Kale

Agano Jipya

2 Mambo Ya Nyakati 9:15-28 Biblia Habari Njema (BHN)

15. Mfalme Solomoni alitengeneza ngao kubwa 200; kila moja ilipakwa kadiri ya kilo saba za dhahabu iliyofuliwa.

16. Pia alitengeneza ngao ndogondogo 300, kila moja ilipakwa dhahabu ipatayo kilo tatu, halafu mfalme akaziweka katika jengo lililoitwa Nyumba ya Msitu wa Lebanoni.

17. Hali kadhalika mfalme alitengeneza kiti cha enzi kikubwa cha pembe, akakifunikiza dhahabu safi.

18. Kiti hicho kilikuwa na ngazi sita na kiti cha kuegemea miguu cha dhahabu, vyote hivyo vilikuwa vimeshikamanishwa na kiti hicho cha enzi; na kila upande kilikuwa na mahali pa kuegemeza mikono; pia kilikuwa na sanamu mbili za simba karibu na mahali hapo pa kuegemeza mikono.

19. Palikuwa na sanamu kumi na mbili za simba waliosimama mwishoni mwa kila ngazi. Kiti kama hicho kilikuwa hakijawahi kutengenezwa katika ufalme wowote ule.

20. Vikombe vyote vya mfalme Solomoni vilikuwa vya dhahabu, na vyombo vyote vilivyokuwa katika Nyumba ya Msitu wa Lebanoni vilikuwa vya dhahabu safi. Fedha haikuhesabiwa kuwa kitu cha thamani katika siku za Solomoni.

21. Solomoni alikuwa na merikebu zilizosafiri mpaka Tarshishi na watumishi wa Huramu, na kila baada ya miaka mitatu, merikebu hizo zilirudi zikimletea dhahabu, fedha, pembe, nyani na tausi.

22. Mfalme Solomoni aliwapita wafalme wote duniani kwa mali na kwa hekima.

23. Nao wafalme wa nchi zote walikuwa na hamu ya kumwendea Solomoni ili kusikiliza hekima yake ambayo Mungu alikuwa amemjalia.

24. Kila mmoja wao alimletea zawadi: Vyombo vya fedha na vya dhahabu, mavazi na silaha manukato, farasi na nyumbu. Zawadi hizi alizipokea kila mwaka.

25. Mfalme Solomoni akawa na vibanda 4,000 vya kuwekea farasi na magari, na askari wapandafarasi 12,000 ambao aliwaweka katika miji yenye vituo vya magari ya farasi na katika Yerusalemu.

26. Aliwatawala wafalme wote waliokuwako kuanzia mto Eufrate, hadi nchi ya Wafilisti na hadi mpakani na Misri.

27. Basi Solomoni alifanya fedha katika Yerusalemu kuwa kitu cha kawaida kama mawe katika Yerusalemu, na mbao za mierezi zilipatikana kwa wingi kama mikuyu iliyomo Shefela.

28. Solomoni aliletewa farasi walionunuliwa kutoka Misri na nchi nyinginezo.

Kusoma sura kamili 2 Mambo Ya Nyakati 9