Agano la Kale

Agano Jipya

1 Wafalme 17:1-13 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Basi Elia wa kijiji cha Tishbe huko Gileadi, akamwambia mfalme Ahabu, “Ninaapa kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli aliye hai ambaye mimi ninamtumikia: Hakutakuwa na umande wala mvua mpaka nitakapotoa amri.”

2. Kisha, neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Elia:

3. “Ondoka hapa uelekee mashariki, ukajifiche penye kijito cha Kerithi kilichoko mashariki ya mto Yordani.

4. Huko, utapata maji ya kunywa katika kijito hicho tena nimewaamuru kunguru wakuletee chakula.”

5. Basi, Elia akatii agizo la Mwenyezi-Mungu, akaenda kukaa kwenye kijito cha Kerithi kilichoko mashariki ya mto Yordani.

6. Kunguru wakawa wanamletea mkate na nyama, asubuhi na jioni; akapata na maji ya kunywa katika kijito hicho.

7. Lakini, baada ya siku chache kijito kikakauka kwa sababu hapakunyesha mvua nchini.

8. Hapo, neno la Mwenyezi-Mungu, lilimjia Elia:

9. “Ondoka uende mjini Sarefathi, karibu na Sidoni, ukae huko. Nimemwamuru mwanamke mmoja mjane akupatie chakula huko.”

10. Basi, Elia akaondoka, akaenda Sarefathi. Alipofika penye lango la mji, alimkuta mwanamke mmoja mjane anaokota kuni. Elia akamwita mwanamke huyo na kumwambia “Niletee maji ninywe.”

11. Yule mwanamke alipokuwa anaondoka, Elia akamwita tena na kumwambia, “Niletee na kipande cha mkate pia.”

12. Huyo mwanamke akamwambia, “Nakuapia kwa jina la Mwenyezi-Mungu, Mungu wako aliye hai, sina mkate hata kidogo. Nilicho nacho ni konzi ya unga katika chungu na mafuta kidogo katika chupa. Nimefika hapa kuokota kuni, kisha niende nyumbani kupika chakula hicho, mwanangu na mimi tule, kisha tufe.”

13. Elia akamwambia, “Usiogope. Nenda ukafanye kama ulivyosema. Lakini nitengenezee mimi kwanza na kuniletea andazi dogo, kisha jitengenezee wewe na mwanao chakula.

Kusoma sura kamili 1 Wafalme 17