Agano la Kale

Agano Jipya

1 Samueli 15:27-35 Biblia Habari Njema (BHN)

27. Samueli alipogeuka ili aende zake, Shauli akashika pindo la vazi lake, nalo likapasuka.

28. Ndipo Samueli alipomwambia Shauli, “Tangu leo Mwenyezi-Mungu ameurarua ufalme wa Israeli kutoka kwako na atampa mtu mwingine miongoni mwa jirani zako aliye bora kuliko wewe.

29. Na Mungu ambaye ni utukufu wa Israeli hadanganyi, wala habadili wazo lake. Yeye si binadamu hata abadili mawazo.”

30. Shauli akajibu, “Nimefanya dhambi. Hata hivyo, unistahi sasa mbele ya wazee wa watu wangu na Waisraeli. Niruhusu nirudi pamoja nawe ili nikamwabudu Mwenyezi-Mungu, Mungu wako.”

31. Basi, Samueli akarudi pamoja naye mpaka Gilgali na Shauli akamwabudu Mwenyezi-Mungu.

32. Kisha Samueli akasema, “Nileteeni hapa Agagi mfalme wa Waamaleki.” Agagi akamwendea Samueli akiwa mwenye furaha kwani alifikiri, “Uchungu wa kifo umepita.”

33. Samueli akasema, “Kwa kuwa upanga wako umewafanya akina mama wengi wasiwe na watoto, ndivyo na mama yako atakavyokuwa bila mtoto miongoni mwa akina mama.” Akamkatakata Agagi vipandevipande mbele ya Mwenyezi-Mungu huko Gilgali.

34. Kisha, Samueli akaenda Rama; na mfalme Shauli akarudi nyumbani kwake huko Gibea.

35. Tangu siku hiyo, Samueli hakumwona tena Shauli, mpaka siku alipofariki. Hata hivyo Samueli alimlilia Shauli. Naye Mwenyezi-Mungu alisikitika kwamba alikuwa amemtawaza Shauli mfalme juu ya Israeli.

Kusoma sura kamili 1 Samueli 15