Agano la Kale

Agano Jipya

1 Mambo Ya Nyakati 19:8-19 Biblia Habari Njema (BHN)

8. Naye Daudi aliposikia habari hizo alimtuma Yoabu na jeshi lote la mashujaa.

9. Waamoni walitoka wakajipanga kwenye lango la mji, hali wale wafalme waliokuja walikuwa peke yao kwenye tambarare.

10. Yoabu alipoona kuwa vita ni vikali dhidi yake, mbele na nyuma, aliwateua baadhi ya wanajeshi hodari zaidi wa Waisraeli, akawapanga kukabiliana na Waaramu.

11. Wale wanajeshi wengine waliobaki, aliwaweka chini ya uongozi wa Abishai ndugu yake, naye akawapanga ili wakabiliane na Waamoni.

12. Yoabu akamwambia Abishai, “Ikiwa Waaramu wananizidi nguvu, utanisaidia; lakini kama Waamoni wanakuzidi nguvu, nitakuja kukusaidia.

13. Basi jipe moyo! Tupigane kiume kwa ajili ya watu wetu, na kwa ajili ya miji ya Mungu wetu; na Mwenyezi-Mungu atutendee lile analoona ni jema kwake.”

14. Basi, Yoabu na watu wake walisonga mbele kupigana na Wasiria; nao Waaramu walikimbia.

15. Waamoni walipoona Waaramu wamekimbia, nao walimkimbia Abishai, nduguye Yoabu, wakaingia mjini. Ndipo Yoabu akarudi Yerusalemu.

16. Lakini Waaramu walipoona ya kwamba wameshindwa na Waisraeli, walituma wajumbe waende kuwaleta Waaramu wengine waliokuwa ngambo ya mto Eufrate wakiongozwa na Shofaki, kamanda wa jeshi la Hadadezeri.

17. Daudi alipopata habari, aliwakusanya pamoja Waisraeli wote, akavuka mto Yordani, akawaendea, akapanga vikosi vyake dhidi yao. Daudi alipopanga vita dhidi ya Wasiria, basi nao walipigana naye.

18. Lakini Waaramu walikimbia mbele ya Waisraeli. Daudi aliwaua Waaramu waendeshao magari 7,000 na askari wa miguu 40,000. Pia alimuua Shofaki, kamanda wa jeshi lao.

19. Kisha watumishi wa Hadadezeri walipoona kuwa wameshindwa na Waisraeli, walifanya mapatano ya amani na Daudi nao wakawa watumishi wa Daudi. Hivyo Waaramu hawakukubali kuwasaidia Waamoni tena.

Kusoma sura kamili 1 Mambo Ya Nyakati 19