Sura

  1. 1
  2. 2
  3. 3
  4. 4

Agano la Kale

Agano Jipya

Wakolosai 1 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Mimi Paulo, mtume wa Kristo Yesu kwa mapenzi ya Mungu, na ndugu Timotheo,

2. tunawaandikia nyinyi watu wa Mungu huko Kolosai, ndugu zetu waaminifu katika kuungana na Kristo. Tunawatakieni neema na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu.

Sala ya shukrani

3. Daima tunamshukuru Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, wakati tunapowaombea.

4. Maana tumesikia juu ya imani yenu kwa Kristo Yesu na juu ya mapendo yenu kwa watu wote wa Mungu.

5. Imani yenu na mapendo yenu vina msingi katika tumaini mlilowekewa mbinguni. Mlipata kusikia juu ya hilo tumaini mara ya kwanza wakati mlipohubiriwa ule ujumbe wa ukweli wa Habari Njema.

6. Injili inazidi kuzaa matunda na kuenea ulimwenguni kote kama vile ilivyofanya kwenu nyinyi tangu siku ile mliposikia juu ya neema ya Mungu na kuitambua ilivyo kweli.

7. Mlijifunza juu ya neema ya Mungu kutoka kwa Epafra, mtumishi mwenzetu, ambaye ni mfanyakazi mwaminifu wa Kristo kwa niaba yetu.

8. Yeye alitupa habari za upendo wenu mliojaliwa na Roho.

9. Kwa sababu hiyo tumekuwa tukiwaombeeni daima tangu wakati tulipopata habari zenu. Tunamwomba Mungu awajazeni ujuzi kamili wa matakwa yake, pamoja na hekima yote na ujuzi wa kiroho.

10. Hapo mtaweza kuishi kama anavyotaka Bwana na kutenda daima yanayompendeza. Maisha yenu yatakuwa yenye matunda ya kila namna ya matendo mema na mtazidi kukua katika kumjua Mungu.

11. Mungu awajalieni nguvu kwa uwezo wake mtukufu ili muweze kustahimili kila kitu kwa uvumilivu.

12. Na kwa furaha mshukuruni Baba, aliyewawezesha nyinyi kuwa na sehemu yenu katika mambo yale aliyowawekea watu wake katika ufalme wa mwanga.

13. Yeye alituokoa katika nguvu ya giza, akatuleta salama katika ufalme wa Mwanae mpenzi.

14. Kwake yeye tunakombolewa, yaani dhambi zetu zinaondolewa.

Kristo na kazi yake

15. Kristo ni mfano wa Mungu asiyeonekana;ni mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote.

16. Maana kwake vitu vyote viliumbwakila kitu duniani na mbinguni,vitu vinavyoonekana na visivyoonekana:Wenye enzi, watawala, wakuu na wenye nguvu.Vyote viliumbwa kwake na kwa ajili yake.

17. Yeye alikuwako kabla ya vitu vyote;vyote huendelea kuwako kwa uwezo wake.

18. Yeye ni kichwa cha mwili wake, yaani kanisa;yeye ni chanzo cha uhai wa huo mwili.Yeye ndiye mwanzo,mzaliwa wa kwanza aliyefufuliwa kutoka kwa wafu,ili awe na nafasi ya kwanza katika vitu vyote.

19. Maana Mungu alipenda utimilifu wake wote uwe ndani yake.

20. Kwake vitu vyote vilipatanishwa na Mungu:Na kwa damu yake msalabani akafanya amanina vitu vyote duniani na mbinguni.

21. Hapo kwanza nyinyi pia mlikuwa mbali na Mungu na mlikuwa maadui zake kwa sababu ya fikira zenu na matendo yenu maovu.

22. Lakini sasa, kwa kifo cha Mwanae aliyeishi hapa duniani, Mungu amewapatanisha naye, kusudi awaweke mbele yake mkiwa watakatifu, safi na bila lawama.

23. Mnapaswa, lakini kuendelea na msingi imara katika imani, wala msikubali kutikiswa kutoka katika tumaini lile mlilopata wakati mlipoisikia Injili. Mimi Paulo nimekuwa mtumishi wa hiyo Injili ambayo imekwisha hubiriwa kila mtu duniani.

Huduma ya Paulo katika makanisa

24. Na sasa nafurahi kuteseka kwa ajili yenu, maana kwa mateso yangu hapa duniani, nasaidia kukamilisha kile kilichopungua bado katika mateso ya Kristo kwa ajili ya mwili wake, yaani kanisa.

25. Nami nimefanywa kuwa mtumishi wa kanisa kufuatana na mpango wake Mungu ambao alinikabidhi kwa faida yenu. Mpango wenyewe ni kuutangaza kwa ukamilifu ujumbe wake,

26. ambao ni siri aliyowaficha binadamu wote tangu milele, lakini sasa amewajulisha watu wake.

27. Mungu ametaka kuwajulisha hao jinsi siri hiyo ilivyo kuu na tukufu ambayo imeenea kwa watu wa mataifa, nayo ndiyo hii: Kristo yuko ndani yenu, na jambo hilo lamaanisha kwamba nyinyi mtaushiriki utukufu wa Mungu.

28. Kwa sababu hiyo tunamhubiri Kristo kwa watu wote; tunawaonya na kuwafundisha wote kwa hekima yote, ili tuweze kumleta kila mmoja mbele ya Mungu akiwa amekomaa katika kuungana na Kristo.

29. Kwa madhumuni hayo mimi nafanya kazi na kujitahidi nikiitumia nguvu kuu ya Kristo ifanyayo kazi ndani yangu.