Agano la Kale

Agano Jipya

Ufunuo 2:4-19 Biblia Habari Njema (BHN)

4. Lakini ninalo jambo moja dhidi yako: Wewe hunipendi tena sasa kama pale awali.

5. Basi, pakumbuke pale ulipokuwa kabla ya kuanguka, ukatubu na kufanya kama ulivyofanya pale awali. La sivyo, naja kwako na kukiondoa kinara chako cha taa mahali pake.

6. Lakini nakusifu juu ya kitu kimoja: Wewe unayachukia wanayoyatenda Wanikolai kama ninavyoyachukia mimi.

7. “Aliye na masikio, basi, na asikie yale Roho anayoyaambia makanisa!“Mshindi nitamjalia kula matunda ya mti wa uhai ulioko ndani ya bustani ya Mungu.

8. “Kwa malaika wa kanisa la Smurna andika:“Mimi niliye wa kwanza na wa mwisho, ambaye nilikufa na kuishi tena, nasema hivi:

9. Najua taabu zako; najua pia umaskini wako, ingawaje kwa kweli wewe ni tajiri; najua kashfa walizokufanyia wale wanaojiita Wayahudi lakini si Wayahudi wa kweli, bali ni kundi lake Shetani.

10. Usiogope hata kidogo yale ambayo itakulazimu kuteseka. Sikiliza! Ibilisi anataka kuwajaribu kwa kuwatia baadhi yenu gerezani; nanyi mtapata dhiki kwa muda wa siku kumi. Muwe waaminifu hata mpaka kufa, nami nitawapeni taji ya uhai.

11. “Aliye na masikio, basi, na asikie yale Roho anayoyaambia makanisa!“Mshindi hataumizwa na kifo cha pili.

12. “Kwa malaika wa kanisa la Pergamumu andika:“Mimi niliye na upanga mkali wenye makali kuwili nasema hivi:

13. Najua unakoishi: Wewe unaishi kwenye makao makuu ya Shetani! Lakini bado unashikilia jina langu; hukuikana imani yako kwangu hata siku zile Antipa, shahidi wangu mwaminifu, alipouawa pale mahali anapoishi Shetani.

14. Lakini ninayo machache dhidi yako: Baadhi yenu ni wafuasi wa Balaamu aliyemfundisha Balaki kuwatega wana wa Israeli wale vyakula vilivyotambikiwa sanamu na kufanya uzinzi.

15. Vivyo hivyo, wako pia miongoni mwenu watu wanaofuata mafundisho ya Wanikolai.

16. Basi, tubu. La sivyo, nitakuja kwako upesi na kupigana na watu hao kwa upanga utokao kinywani mwangu.

17. “Aliye na masikio, basi, na asikie yale Roho anayoyaambia makanisa!“Mshindi nitampa ile mana iliyofichika. Nitampa pia jiwe jeupe lililoandikwa jina jipya ambalo hakuna mtu aliyelijua isipokuwa tu wale wanaolipokea.

18. “Kwa malaika wa kanisa la Thuatira andika hivi:“Huu ndio ujumbe wa Mwana wa Mungu, ambaye macho yake yametameta kama moto, na miguu yake inang'aa kama shaba iliyosuguliwa.

19. Najua mambo yako yote. Najua upendo wako, imani yako, utumishi wako na uvumilivu wako. Wewe unafanya vizuri zaidi sasa kuliko pale awali.

Kusoma sura kamili Ufunuo 2