Agano la Kale

Agano Jipya

Ufunuo 2:1-11 Biblia Habari Njema (BHN)

1. “Kwa malaika wa kanisa la Efeso andika: “Mimi nishikaye zile nyota saba katika mkono wangu wa kulia na ambaye hutembea katikati ya vinara saba vya taa vya dhahabu, nasema hivi:

2. Najua mambo yako yote; najua bidii yako na uvumilivu wako. Najua kwamba huwezi kuwavumilia watu waovu, na kwamba umewapima wale wanaojisemea kuwa mitume na kumbe sio, ukagundua kwamba ni waongo.

3. Wewe unayo saburi, umestahimili taabu nyingi kwa ajili ya jina langu, wala hukuvunjika moyo.

4. Lakini ninalo jambo moja dhidi yako: Wewe hunipendi tena sasa kama pale awali.

5. Basi, pakumbuke pale ulipokuwa kabla ya kuanguka, ukatubu na kufanya kama ulivyofanya pale awali. La sivyo, naja kwako na kukiondoa kinara chako cha taa mahali pake.

6. Lakini nakusifu juu ya kitu kimoja: Wewe unayachukia wanayoyatenda Wanikolai kama ninavyoyachukia mimi.

7. “Aliye na masikio, basi, na asikie yale Roho anayoyaambia makanisa!“Mshindi nitamjalia kula matunda ya mti wa uhai ulioko ndani ya bustani ya Mungu.

8. “Kwa malaika wa kanisa la Smurna andika:“Mimi niliye wa kwanza na wa mwisho, ambaye nilikufa na kuishi tena, nasema hivi:

9. Najua taabu zako; najua pia umaskini wako, ingawaje kwa kweli wewe ni tajiri; najua kashfa walizokufanyia wale wanaojiita Wayahudi lakini si Wayahudi wa kweli, bali ni kundi lake Shetani.

10. Usiogope hata kidogo yale ambayo itakulazimu kuteseka. Sikiliza! Ibilisi anataka kuwajaribu kwa kuwatia baadhi yenu gerezani; nanyi mtapata dhiki kwa muda wa siku kumi. Muwe waaminifu hata mpaka kufa, nami nitawapeni taji ya uhai.

11. “Aliye na masikio, basi, na asikie yale Roho anayoyaambia makanisa!“Mshindi hataumizwa na kifo cha pili.

Kusoma sura kamili Ufunuo 2