Agano la Kale

Agano Jipya

Ufunuo 11:8-19 Biblia Habari Njema (BHN)

8. Maiti zao zitabaki katika barabara za mji mkuu ambapo Bwana wao alisulubiwa. Jina la kupanga la mji huo ni Sodoma au Misri.

9. Watu wa kila kabila, lugha, taifa na rangi wataziangalia maiti hizo kwa muda wa siku tatu na nusu, na hawataruhusu zizikwe.

10. Watu waishio duniani watafurahia kifo cha hao wawili. Watafanya sherehe na kupelekeana zawadi, maana manabii hawa wawili walikuwa wamewasumbua mno watu wa dunia.

11. Lakini baada ya zile siku tatu na nusu pumzi ya uhai kutoka kwa Mungu iliwaingia, nao wakasimama; wote waliowaona wakaingiwa na hofu kuu.

12. Kisha, hao manabii wawili wakasikia sauti kubwa kutoka mbinguni ikiwaambia, “Njoni hapa juu!” Nao wakapanda juu mbinguni katika wingu, maadui zao wakiwa wanawatazama.

13. Wakati huohuo, kukatokea tetemeko kubwa la ardhi, sehemu moja ya kumi ya ardhi ikaharibiwa. Watu 7,000 wakauawa kwa tetemeko hilo la ardhi. Watu waliosalia wakaogopa sana, wakamtukuza Mungu wa mbinguni.

14. Maafa ya pili yamepita; lakini tazama! Maafa ya tatu yanafuata hima.

15. Kisha, malaika wa saba akapiga tarumbeta yake. Na sauti kuu zikasikika mbinguni zikisema, “Sasa ufalme wa ulimwengu ni wa Bwana wetu na Kristo wake. Naye atatawala milele na milele!”

16. Kisha, wale wazee ishirini na wanne walioketi mbele ya Mungu katika viti vyao vya enzi, wakaanguka kifudifudi, wakamwabudu Mungu,

17. wakisema:“Tunakushukuru ee Bwana Mungu Mwenye Nguvu,uliyeko na uliyekuwako!Maana umetumia nguvu yako kuu, ukaanza kutawala!

18. Watu wa mataifa waliwaka hasira,lakini ghadhabu yako imefika,naam wakati wa kuwahukumu wafu.Ndio wakati wa kuwatuza watumishi wako manabii,watakatifu na wote wanaolitukuza jina lako, wakubwa kwa wadogo.Ni wakati wa kuwaangamiza waangamizi wa dunia.”

19. Kisha hekalu la Mungu mbinguni likafunguliwa, na sanduku la agano lake likaonekana hekaluni mwake. Kukatokea umeme, sauti, ngurumo, tetemeko la ardhi, na mvua kubwa ya mawe.

Kusoma sura kamili Ufunuo 11