Agano la Kale

Agano Jipya

Mathayo 27:54-66 Biblia Habari Njema (BHN)

54. Basi, jemadari na wale waliokuwa wakimlinda Yesu walipoona tetemeko la ardhi na yale mambo yaliyotukia, wakaogopa sana, wakasema, “Hakika mtu huyu alikuwa Mwana wa Mungu.”

55. Mahali hapo walikuwapo wanawake wengi wakitazama kwa mbali. Hao ndio wale waliomfuata Yesu kutoka Galilaya wakimtumikia.

56. Miongoni mwao walikuwa Maria Magdalene, Maria mama yao Yakobo na Yosefu, pamoja na mama yao wana wa Zebedayo.

57. Ilipokuwa jioni, akaja mtu mmoja tajiri mwenyeji wa Arimathaya, jina lake Yosefu. Yeye pia alikuwa mwanafunzi wa Yesu.

58. Akamwendea Pilato, akaomba apewe mwili wa Yesu. Basi, Pilato akaamuru apewe.

59. Yosefu akauchukua ule mwili, akauzungushia sanda safi ya kitani,

60. akauweka ndani ya kaburi lake jipya alilokuwa amelichonga katika mwamba. Kisha akavingirisha jiwe kubwa mbele ya mlango wa kaburi, akaenda zake.

61. Maria Magdalene na yule Maria mwingine walikuwa wameketi kulielekea kaburi.

62. Kesho yake, yaani siku iliyofuata ile ya Maandalio, makuhani wakuu na Mafarisayo walimwendea Pilato,

63. Wakasema, “Mheshimiwa, tunakumbuka kwamba yule mdanganyifu alisema kabla ya kufa ati, ‘Baada ya siku tatu nitafufuka.’

64. Kwa hiyo amuru kaburi lilindwe mpaka siku ya tatu ili wanafunzi wake wasije wakamwiba na kuwaambia watu kwamba amefufuka. Uongo huu wa mwisho utakuwa mbaya zaidi kuliko ule wa awali.”

65. Pilato akawaambia, “Haya, mnao walinzi; nendeni mkalinde kadiri mjuavyo.”

66. Basi, wakaenda, wakalilinda kaburi, wakatia mhuri juu ya lile jiwe na kuacha hapo askari walinzi.

Kusoma sura kamili Mathayo 27