Agano la Kale

Agano Jipya

Mathayo 27:33-53 Biblia Habari Njema (BHN)

33. Walipofika mahali paitwapo Golgotha, maana yake, mahali pa Fuvu la Kichwa,

34. wakampa mchanganyiko wa divai na kitu kichungu. Lakini Yesu alipoonja akakataa kunywa.

35. Walimsulubisha, kisha wakagawana mavazi yake kwa kuyapigia kura.

36. Wakaketi, wakawa wanamchunga.

37. Juu ya kichwa chake wakaweka shtaka dhidi yake lililoandikwa, “Huyu ni Yesu, Mfalme wa Wayahudi.”

38. Wanyanganyi wawili walisulubiwa pia pamoja naye, mmoja upande wa kushoto na mwingine upande wa kulia.

39. Watu waliokuwa wanapita mahali hapo walimtukana wakitikisa vichwa vyao na kusema,

40. “Wewe! Si ulijidai kulivunja hekalu na kulijenga kwa siku tatu? Sasa jiokoe mwenyewe. Kama wewe ni Mwana wa Mungu, basi, shuka msalabani!”

41. Hali kadhalika na makuhani wakuu pamoja na waalimu wa sheria na wazee walimdhihaki wakisema,

42. “Aliwaokoa wengine, lakini kujiokoa mwenyewe hawezi! Ati yeye ni mfalme wa Wayahudi! Basi, sasa na ashuke msalabani, nasi tutamwamini.

43. Alimtumainia Mungu na kusema ati yeye ni Mwana wa Mungu; basi, Mungu na amwokoe kama anamtaka.”

44. Hali kadhalika na wale waliosulubiwa pamoja naye wakamtukana.

45. Tangu saa sita mchana mpaka saa tisa, giza likaikumba nchi yote.

46. Mnamo saa tisa Yesu akalia kwa sauti kubwa, “Eli, Eli, lema sabakthani?” Maana yake, “Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?”

47. Lakini wale waliosimama pale waliposikia hivyo wakasema, “Anamwita Elia.”

48. Mmoja wao akakimbia, akachukua sifongo, akaichovya katika siki, akaiweka juu ya mwanzi, akampa anywe.

49. Wengine wakasema, “Acha tuone kama Elia anakuja kumwokoa.”

50. Basi, Yesu akalia tena kwa sauti kubwa, akakata roho.

51. Hapo pazia la hekalu likapasuka vipande viwili, toka juu mpaka chini; nchi ikatetemeka; miamba ikapasuka;

52. makaburi yakafunguka na watu wengi wa Mungu waliokufa wakafufuliwa;

53. nao, baada ya kufufuka kwake, wakatoka makaburini, wakaingia katika mji mtakatifu, wakaonekana na watu wengi.

Kusoma sura kamili Mathayo 27