Agano la Kale

Agano Jipya

Mathayo 24:32-43 Biblia Habari Njema (BHN)

32. “Kwa mtini jifunzeni mfano huu: Mara tu matawi yake yanapoanza kuwa laini na kuchanua majani, mnajua kwamba wakati wa mavuno umekaribia.

33. Hali kadhalika nanyi mtakapoona mambo haya yote yakitendeka, jueni kwamba yuko karibu sana.

34. Nawaambieni kweli, kizazi hiki hakitapita kabla ya mambo hayo yote kutukia.

35. Mbingu na dunia zitapita, lakini maneno yangu hayatapita kamwe.

36. “Lakini, juu ya siku au saa hiyo, hakuna mtu ajuaye itakuja lini; wala malaika wa mbinguni, wala Mwana; Baba peke yake ndiye ajuaye.

37. Kwa maana kama ilivyokuwa nyakati za Noa, ndivyo itakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Mtu.

38. Maana nyakati hizo, kabla ya gharika kuu, watu walikuwa wakila na kunywa, wakioa na kuolewa, mpaka Noa alipoingia ndani ya ile safina.

39. Hawakujua kuna nini mpaka ile gharika ilipotokea, ikawakumba wote. Ndivyo itakavyokuwa wakati Mwana wa Mtu atakapokuja.

40. Wakati huo watu wawili watakuwa shambani; mmoja atachukuliwa na mwingine ataachwa.

41. Kina mama wawili watakuwa wanasaga nafaka, mmoja atachukuliwa na mwingine ataachwa.

42. Basi, kesheni, kwa maana hamjui siku atakayokuja Bwana wenu.

43. Lakini kumbukeni jambo hili: Kama mwenye nyumba angejua siku mwizi atakapofika, angekesha, wala hangeiacha nyumba yake ivunjwe.

Kusoma sura kamili Mathayo 24