Agano la Kale

Agano Jipya

Marko 8:7-20 Biblia Habari Njema (BHN)

7. Walikuwa pia na visamaki vichache. Yesu akavibariki, akaamuru vigawiwe watu vilevile.

8. Watu wakala, wakashiba. Wakakusanya makombo wakajaza vikapu saba.

9. Nao waliokula walikuwa watu wapatao 4,000. Yesu akawaaga,

10. na mara akapanda mashua pamoja na wanafunzi wake, akaenda wilaya ya Dalmanutha.

11. Mafarisayo walikuja, wakaanza kujadiliana na Yesu. Kwa kumjaribu, wakamtaka afanye ishara kutoka mbinguni.

12. Yesu akahuzunika rohoni, akasema, “Mbona kizazi hiki kinataka ishara? Kweli nawaambieni, kizazi hiki hakitapewa ishara yoyote.”

13. Basi, akawaacha, akapanda tena mashua, akaanza safari kwenda ngambo ya pili ya ziwa.

14. Wanafunzi walikuwa wamesahau kuchukua mikate; walikuwa na mkate mmoja tu katika mashua.

15. Yesu akawaonya, “Angalieni sana! Jihadharini na chachu ya Mafarisayo na chachu ya Herode.”

16. Wanafunzi wakaanza kujadiliana wao kwa wao, “Anasema hivyo kwa kuwa hatuna mikate.”

17. Yesu alitambua hayo, akawaambia, “Mbona mnajadiliana juu ya kutokuwa na mikate? Je, bado hamjafahamu, wala hamjaelewa? Je, mioyo yenu ni mizito?

18. Je, mnayo macho na hamwoni? Mnayo masikio na hamsikii? Je, hamkumbuki

19. wakati ule nilipoimega ile mikate mitano na kuwapa watu 5,000? Mlikusanya vikapu vingapi vya mabaki.” Wakamjibu, “Kumi na viwili.”

20. “Na nilipoimega ile mikate saba na kuwapa watu 4,000, mlikusanya vikapu vingapi vya mabaki?” Wakamjibu, “Saba.”

Kusoma sura kamili Marko 8