Agano la Kale

Agano Jipya

Marko 13:21-31 Biblia Habari Njema (BHN)

21. “Basi mtu akiwaambieni, ‘Tazama, Kristo yupo hapa,’ au ‘Yupo pale,’ msimsadiki.

22. Maana watatokea kina Kristo wa uongo na manabii wa uongo, watafanya ishara na maajabu, kwa ajili ya kuwapotosha wateule wa Mungu kama ikiwezekana.

23. Lakini nyinyi jihadharini. Mimi nimewaambieni mambo yote kabla hayajatokea.

24. “Basi, siku hizo, baada ya dhiki hiyo, jua litatiwa giza na mwezi hautaangaza.

25. Nyota zitaanguka kutoka angani, na nguvu za mbingu zitatikiswa.

26. Hapo watamwona Mwana wa Mtu akija katika mawingu kwa nguvu nyingi na utukufu.

27. Kisha atawatuma malaika wake wawakusanye wateule wake kutoka pande zote nne za dunia, kutoka mwisho wa dunia mpaka mwisho wa mbingu.

28. “Kwa mtini jifunzeni mfano huu: Mara tu matawi yake yanapoanza kuwa laini na kuchanua majani, mnajua kwamba wakati wa mavuno umekaribia.

29. Hali kadhalika nanyi mtakapoona mambo hayo yakitendeka, jueni kwamba Mwana wa Mtu yuko karibu sana.

30. Nawaambieni kweli, kizazi hiki hakitapita kabla ya mambo hayo yote kutukia.

31. Mbingu na dunia zitapita, lakini maneno yangu hayatapita kamwe.

Kusoma sura kamili Marko 13