Agano la Kale

Agano Jipya

Marko 10:8-23 Biblia Habari Njema (BHN)

8. nao wawili watakuwa mwili mmoja. Kwa hiyo, wao si wawili tena bali mwili mmoja.

9. Basi, alichounganisha Mungu, binadamu asitenganishe.”

10. Walipoingia tena ndani ya nyumba, wanafunzi wake walimwuliza juu ya jambo hilo.

11. Naye akawaambia, “Anayemwacha mkewe na kuoa mwingine, anazini dhidi ya mkewe.

12. Na mwanamke anayemwacha mumewe na kuolewa na mwingine anazini.”

13. Watu walimletea Yesu watoto wadogo ili awaguse, lakini wanafunzi wakawakemea.

14. Yesu alipoona hivyo, alikasirika akawaambia, “Waacheni hao watoto waje kwangu, wala msiwazuie, kwa maana ufalme wa Mungu ni kwa ajili ya watu walio kama watoto hawa.

15. Nawaambieni kweli, mtu yeyote asiyeupokea ufalme wa Mungu kama mtoto mdogo hataingia humo.”

16. Kisha akawapokea watoto hao, akawawekea mikono, akawabariki.

17. Yesu alipoanza tena safari yake, mtu mmoja alimjia mbio, akapiga magoti mbele yake, akamwuliza, “Mwalimu mwema, nifanyeje niupate uhai wa milele?”

18. Yesu akamjibu, “Mbona unaniita mwema? Hakuna aliye mwema ila Mungu peke yake.

19. Unazijua amri: ‘Usizini, Usiue, Usiibe, Usitoe ushahidi wa uongo, Usidanganye, Waheshimu baba yako na mama yako.’”

20. Naye akamjibu, “Mwalimu, hayo yote nimeyazingatia tangu ujana wangu.”

21. Yesu akamtazama, akampenda, akamwambia, “Umepungukiwa na kitu kimoja: Nenda ukauze kila kitu ulicho nacho, uwape maskini hizo fedha, nawe utakuwa na hazina mbinguni, kisha uje unifuate.”

22. Aliposikia hayo, alisikitika, akaenda zake akiwa na huzuni, kwa maana alikuwa na mali nyingi.

23. Yesu akatazama pande zote, akawaambia wanafunzi wake, “Jinsi gani itakavyokuwa vigumu kwa matajiri kuingia katika ufalme wa Mungu!”

Kusoma sura kamili Marko 10