Agano la Kale

Agano Jipya

Marko 1:23-42 Biblia Habari Njema (BHN)

23. Mara akatokea mle ndani ya sunagogi mtu mmoja mwenye pepo mchafu,

24. akapaza sauti, “Una nini nasi, wewe Yesu wa Nazareti? Je, umekuja kutuangamiza? Najua wewe ni nani: Wewe ni Mtakatifu wa Mungu!”

25. Yesu akamkemea huyo pepo akisema, “Nyamaza! Mtoke mtu huyu.”

26. Basi, huyo pepo mchafu akamtikisatikisa mtu huyo, kisha akalia kwa sauti kubwa, akamtoka.

27. Watu wote wakashangaa, wakaulizana, “Ni mambo gani haya? Je, ni mafundisho mapya? Mtu huyu anayo mamlaka ya kuamuru hata pepo wachafu, nao wanamtii!”

28. Habari za Yesu zikaenea upesi kila mahali katika eneo la Galilaya.

29. Wakatoka katika sunagogi, wakaenda moja kwa moja hadi nyumbani kwa Simoni na Andrea; Yakobo na Yohane walikwenda pamoja nao.

30. Basi, mama mmoja, mkwewe Simoni, alikuwa kitandani ana homa kali. Wakamwarifu Yesu mara alipowasili.

31. Yesu akamwendea huyo mama, akamshika mkono, akamwinua. Na ile homa ikamwacha, akaanza kuwatumikia.

32. Jioni, jua lilipokwisha tua, wakamletea Yesu wagonjwa wote na watu waliopagawa na pepo.

33. Watu wote wa mji ule wakakusanyika nje ya mlango.

34. Naye Yesu akawaponya watu wengi waliokuwa na magonjwa mbalimbali; aliwafukuza pepo wengi, lakini hakuwaruhusu kusema kitu maana walikuwa wanamjua yeye ni nani.

35. Kesho yake, kabla ya mapambazuko, Yesu alitoka, akaenda mahali pa faragha kusali.

36. Simoni na wenzake wakaenda kumtafuta.

37. Walipomwona, wakamwambia, “Kila mtu anakutafuta.”

38. Yesu akawaambia, “Twendeni katika miji mingine ya jirani nikahubiri huko pia, maana nimekuja kwa sababu hiyo.”

39. Basi, akaenda kila mahali huko Galilaya akihubiri katika masunagogi na kufukuza pepo.

40. Mtu mmoja mwenye ukoma alimwendea Yesu, akapiga magoti, akamwomba: “Ukitaka, waweza kunitakasa!”

41. Yesu akamwonea huruma, akanyosha mkono wake, akamgusa na kumwambia, “Nataka! Takasika!”

42. Mara ukoma ukamwacha mtu huyo, akatakasika.

Kusoma sura kamili Marko 1