Agano la Kale

Agano Jipya

Luka 9:51-62 Biblia Habari Njema (BHN)

51. Wakati ulipokaribia ambapo Yesu angechukuliwa juu mbinguni, yeye alikata shauri kwenda Yerusalemu.

52. Basi, akawatuma wajumbe wamtangulie, nao wakaenda wakaingia kijiji kimoja cha Wasamaria ili wamtayarishie mahali.

53. Lakini wenyeji wa hapo hawakutaka kumpokea kwa sababu alikuwa anaelekea Yerusalemu.

54. Basi, wanafunzi wake, kina Yohane na Yakobo, walipoona hayo, wakasema, “Bwana, wataka tuamuru moto ushuke kutoka mbinguni uwateketeze?”

55. Lakini yeye akawageukia, akawakemea.

56. Wakatoka, wakaenda kijiji kingine.

57. Walipokuwa wakisafiri njiani, mtu mmoja akamwambia Yesu, “Nitakufuata kokote utakakokwenda.”

58. Yesu akasema, “Mbweha wana mapango, na ndege wana viota lakini Mwana wa Mtu hana mahali pa kupumzikia.”

59. Kisha akamwambia mtu mwingine, “Nifuate.” Lakini huyo akasema, “Bwana, niruhusu kwanza niende kumzika baba yangu.”

60. Yesu akamwambia, “Waache wafu wazike wafu wao; bali wewe nenda ukatangaze ufalme wa Mungu.”

61. Na mtu mwingine akamwambia, “Nitakufuata, lakini niruhusu kwanza nikawaage wale walio nyumbani kwangu.”

62. Yesu akamwambia, “Yeyote anayeshika jembe tayari kulima na huku anaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa Mungu.”

Kusoma sura kamili Luka 9