Agano la Kale

Agano Jipya

Luka 6:21-35 Biblia Habari Njema (BHN)

21. Heri nyinyi mnaosikia njaa sasa,maana baadaye mtashiba.Heri nyinyi mnaolia sasa,maana baadaye mtacheka kwa furaha.

22. “Heri yenu nyinyi iwapo watu watawachukia, watawatenga, watawatukana na kuwaharibieni jina kwa ajili ya Mwana wa Mtu.

23. Wakati hayo yatakapotokea, furahini na kucheza, maana hakika tuzo lenu ni kubwa mbinguni. Kwa maana wazee wao waliwatendea manabii vivyo hivyo.

24. Lakini ole wenu nyinyi mlio matajiri,maana mmekwisha pata faraja yenu.

25. Ole wenu nyinyi mnaoshiba sasa,maana baadaye mtasikia njaa.Ole wenu nyinyi mnaocheka kwa furaha sasa,maana baadaye mtaomboleza na kulia.

26. Ole wenu nyinyi iwapo watu wote wanawasifu,maana wazee wao waliwafanyia manabii wa uongo vivyo hivyo.

27. “Lakini nawaambieni nyinyi mnaonisikiliza, wapendeni maadui zenu, watendeeni mema wale wanaowachukieni.

28. Watakieni baraka wale wanaowalaani, na waombeeni wale wanaowatendea vibaya.

29. Mtu akikupiga shavu moja mgeuzie pia la pili. Mtu akikunyanganya koti lako mwachie pia shati lako.

30. Yeyote anayekuomba mpe, na mtu akikunyanganya mali yako usimtake akurudishie.

31. Jinsi mnavyotaka watu wawatendee nyinyi, watendeeni wao vivyo hivyo.

32. “Na ikiwa mnawapenda tu wale wanaowapenda nyinyi, je, mtapata tuzo gani? Hakuna! Kwa maana hata wenye dhambi huwapenda wale wanaowapenda wao.

33. Tena, kama mkiwatendea mema wale tu wanaowatendeeni mema, mtapata tuzo gani? Hata wenye dhambi hufanya hayo.

34. Na kama mnawakopesha wale tu mnaotumaini watawalipeni, je, mtapata tuzo gani? Hata wenye dhambi huwakopesha wenye dhambi wenzao ili warudishiwe kima kilekile.

35. Ila nyinyi wapendeni maadui zenu na kuwatendea mema; kopesheni bila kutazamia kurudishiwa, na tuzo lenu litakuwa kubwa, nanyi mtakuwa watoto wa Mungu aliye juu. Kwa maana yeye ni mwema kwa wale wasio na shukrani na walio wabaya.

Kusoma sura kamili Luka 6