Agano la Kale

Agano Jipya

Luka 6:13-23 Biblia Habari Njema (BHN)

13. Kesho yake aliwaita wanafunzi wake, na miongoni mwao akawachagua watu kumi na wawili ambao aliwaita mitume:

14. Simoni (ambaye Yesu alimpa jina Petro) na Andrea ndugu yake, Yakobo na Yohane, Filipo na Bartholomayo,

15. Mathayo na Thoma, Yakobo wa Alfayo na Simoni (aliyeitwa Zelote),

16. Yuda wa Yakobo na Yuda Iskarioti ambaye baadaye alikuwa msaliti.

17. Baada ya kushuka mlimani pamoja nao, Yesu alisimama mahali palipokuwa tambarare. Hapo kulikuwa na kundi kubwa la wanafunzi wake na umati wa watu waliotoka pande zote za Yudea na Yerusalemu na pwani ya Tiro na Sidoni. Wote walifika kumsikiliza Yesu na kuponywa magonjwa yao.

18. Aliwaponya pia wote waliokuwa wanasumbuliwa na pepo wachafu.

19. Watu wote walitaka kumgusa, kwa maana nguvu ilikuwa inatoka ndani yake na kuwaponya wote.

20. Yesu akawageukia wanafunzi wake, akasema:“Heri nyinyi mlio maskini,maana ufalme wa Mungu ni wenu.

21. Heri nyinyi mnaosikia njaa sasa,maana baadaye mtashiba.Heri nyinyi mnaolia sasa,maana baadaye mtacheka kwa furaha.

22. “Heri yenu nyinyi iwapo watu watawachukia, watawatenga, watawatukana na kuwaharibieni jina kwa ajili ya Mwana wa Mtu.

23. Wakati hayo yatakapotokea, furahini na kucheza, maana hakika tuzo lenu ni kubwa mbinguni. Kwa maana wazee wao waliwatendea manabii vivyo hivyo.

Kusoma sura kamili Luka 6