Agano la Kale

Agano Jipya

Luka 24:1-12 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Jumapili, alfajiri na mapema, wale wanawake walikwenda kaburini wakichukua yale manukato waliyotayarisha.

2. Walikuta lile jiwe limevingirishwa mbali na kaburi.

3. Walipoingia ndani, hawakuuona mwili wa Bwana Yesu.

4. Walipokuwa bado wanashangaa juu ya jambo hilo, mara watu wawili waliovaa mavazi yenye kungaa sana, wakasimama karibu nao.

5. Hao wanawake wakaingiwa na hofu, wakainama chini. Ndipo wale watu wakawaambia, “Kwa nini mnamtafuta aliye hai kati ya wafu?

6. Hayuko hapa; amefufuka. Kumbukeni aliyowaambieni alipokuwa kule Galilaya:

7. ‘Ni lazima Mwana wa Mtu atolewe kwa watu waovu, nao watamsulubisha na siku ya tatu atafufuka.’”

8. Hapo hao wanawake wakayakumbuka maneno yake,

9. wakarudi kutoka kaburini, wakawapa mitume wale kumi na mmoja na wafuasi wengine habari za mambo hayo yote.

10. Hao waliotoa habari hizo kwa mitume ni: Maria Magdalene, Yoana na Maria mama wa Yakobo, pamoja na wanawake wengine walioandamana nao.

11. Mitume waliyachukua maneno hayo kama yasiyo na msingi, hivyo hawakuamini.

12. Lakini Petro alitoka, akaenda mbio hadi kaburini. Alipoinama kuchungulia ndani, akaiona tu ile sanda. Akarudi nyumbani huku akiwa anashangaa juu ya hayo yaliyotokea.

Kusoma sura kamili Luka 24