Agano la Kale

Agano Jipya

Luka 18:17-32 Biblia Habari Njema (BHN)

17. Nawaambieni kweli, mtu yeyote asiyeupokea ufalme wa Mungu kama mtoto mdogo, hataingia katika ufalme huo.”

18. Kiongozi mmoja, Myahudi, alimwuliza Yesu, “Mwalimu mwema, nifanye nini ili niweze kuupata uhai wa milele?”

19. Yesu akamwambia, “Mbona waniita mwema? Hakuna aliye mwema ila Mungu peke yake.

20. Unazijua amri: ‘Usizini; Usiue; Usiibe; Usitoe ushahidi wa uongo; Waheshimu baba yako na mama yako.’”

21. Yeye akasema, “Hayo yote nimeyazingatia tangu ujana wangu.”

22. Yesu aliposikia hayo, akamwambia, “Unatakiwa bado kufanya kitu kimoja: Uza kila kitu ulicho nacho, wagawie maskini hiyo fedha, nawe utakuwa na hazina yako mbinguni; halafu njoo unifuate.”

23. Lakini huyo mtu aliposikia hayo, alihuzunika sana kwa sababu alikuwa tajiri sana.

24. Yesu alipoona akihuzunika hivyo, akasema, “Jinsi gani ilivyo vigumu kwa matajiri kuingia katika ufalme wa Mungu!

25. Naam, ni rahisi zaidi kwa ngamia kupita katika tundu la sindano, kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu.”

26. Wale watu waliposikia hayo, wakasema, “Nani basi, atakayeokolewa?”

27. Yesu akajibu, “Yasiyowezekana kwa binadamu, yanawezekana kwa Mungu.”

28. Naye Petro akamwuliza, “Na sisi, je? Tumeacha vitu vyote tukakufuata!”

29. Yesu akawaambia, “Kweli nawaambieni, mtu yeyote aliyeacha nyumba au mke au ndugu au wazazi au watoto kwa ajili ya ufalme wa Mungu,

30. atapokea mengi zaidi wakati huu wa sasa, na uhai wa milele wakati ujao.”

31. Yesu aliwachukua kando wale kumi na wawili, akawaambia, “Sikilizeni! Tunakwenda Yerusalemu na huko kila kitu kilichoandikwa na manabii kuhusu Mwana wa Mtu kitakamilishwa.

32. Kwa maana atakabidhiwa kwa watu wa mataifa nao watamtendea vibaya na kumtemea mate.

Kusoma sura kamili Luka 18