Agano la Kale

Agano Jipya

Luka 12:28-42 Biblia Habari Njema (BHN)

28. Ikiwa basi, Mungu hulivika hivyo jani la shambani ambalo leo liko na kesho latupwa motoni, je, si atawafanyia nyinyi zaidi? Enyi watu wenye imani haba!

29. “Basi, msivurugike akili, mkihangaika juu ya mtakachokula au mtakachokunywa.

30. Kwa maana hayo yote yanahangaikiwa na watu wote wasiomjua Mungu. Baba yenu anajua kwamba mnahitaji vitu hivyo.

31. Shughulikeni kwanza juu ya ufalme wa Mungu, na hayo mtapewa kwa ziada.

32. “Msiogope, enyi kundi dogo! Maana Baba yenu amependa kuwapeni ufalme.

33. Uzeni mali yenu mkawape maskini hizo fedha. Jifanyieni mifuko isiyochakaa, na kujiwekea hazina mbinguni ambako haitapungua. Huko wezi hawakaribii, wala nondo hawaharibu.

34. Pale ilipo hazina yako, ndipo pia utakapokuwa moyo wako.

35. “Muwe tayari mmejifunga mkanda kiunoni, na taa zenu ziwe zinawaka;

36. muwe kama watumishi wanaomngojea bwana wao arudi kutoka harusini, ili wamfungulie mara atakapobisha.

37. Heri yao watumishi wale ambao bwana wao atakaporudi atawakuta wanakesha! Nawaambieni hakika, huyo bwana atajifunga mkanda kiunoni, atawaketisha mezani na kuwahudumia.

38. Hata kama atarudi usiku wa manane au alfajiri na kuwakuta wanakesha, heri yao watumishi hao!

39. Jueni kwamba, kama mwenye nyumba angejua saa ambayo mwizi atakuja, angekesha, wala hangeiacha nyumba yake ivunjwe.

40. Nanyi, kadhalika muwe tayari, maana Mwana wa Mtu atakuja saa msiyoitazamia.”

41. Petro akamwambia, “Bwana, mfano huo ni kwa ajili yetu tu, au ni kwa ajili ya watu wote?”

42. Bwana akajibu, “Ni nani, basi, aliye mtumishi mwaminifu na mwenye busara, ambaye bwana wake atamweka juu ya watumishi wake ili awape chakula wakati ufaao?

Kusoma sura kamili Luka 12