Agano la Kale

Agano Jipya

Luka 1:35-48 Biblia Habari Njema (BHN)

35. Malaika akamjibu, “Roho Mtakatifu atakushukia, na uwezo wake Mungu Mkuu utakujia kama kivuli; kwa sababu hiyo, mtoto atakayezaliwa ataitwa Mtakatifu, Mwana wa Mungu.

36. Ujue pia kwamba hata Elisabeti, jamaa yako, naye amepata mimba ingawa ni mzee, na sasa ni mwezi wa sita kwake yeye ambaye watu walimfahamu kuwa tasa.

37. Kwa maana hakuna jambo lisilowezekana kwa Mungu.”

38. Maria akasema, “Mimi ni mtumishi wa Bwana, nitendewe kama ulivyosema.” Kisha yule malaika akaenda zake.

39. Siku kadhaa baadaye, Maria alifunga safari akaenda kwa haraka hadi mji mmoja ulioko katika milima ya Yudea.

40. Huko, aliingia katika nyumba ya Zakaria, akamsalimu Elisabeti.

41. Mara tu Elisabeti aliposikia sauti ya Maria, mtoto mchanga tumboni mwake Elisabeti akaruka. Naye Elisabeti akajazwa Roho Mtakatifu,

42. akasema kwa sauti kubwa, “Umebarikiwa kuliko wanawake wote, naye utakayemzaa amebarikiwa.

43. Mimi ni nani hata mama wa Bwana wangu afike kwangu?

44. Nakuambia, mara tu niliposikia sauti yako, mtoto mchanga tumboni mwangu aliruka kwa furaha.

45. Heri yako wewe uliyesadiki kwamba yatatimia yale Bwana aliyokuambia.”

46. Naye Maria akasema,“Moyo wangu wamtukuza Bwana,

47. roho yangu inafurahi kwa sababu ya Mungu Mwokozi wangu.

48. Kwa kuwa amemwangalia kwa huruma mtumishi wake mnyenyekevu.Hivyo tangu sasa watu wote wataniita mwenye heri.

Kusoma sura kamili Luka 1