Agano la Kale

Agano Jipya

Luka 1:27-38 Biblia Habari Njema (BHN)

27. kwa msichana mmoja bikira aitwaye Maria, mchumba wa mtu mmoja jina lake Yosefu, wa ukoo wa Daudi.

28. Malaika akamwendea, akamwambia, “Salamu, ewe uliyejaliwa neema na Mungu! Bwana yuko nawe!”

29. Maria aliposikia maneno hayo alifadhaika sana, akawaza: Maneno hayo yanamaanisha nini?

30. Malaika akamwambia, “Usiogope Maria, kwa maana Mungu amekujalia neema.

31. Utachukua mimba, utamzaa mtoto wa kiume, nawe utampa jina Yesu.

32. Yeye atakuwa mkubwa na ataitwa Mwana wa Mungu Mkuu. Bwana Mungu atampa kiti cha mfalme Daudi, babu yake.

33. Kwa hivyo atautawala ukoo wa Yakobo milele, na ufalme wake hautakuwa na mwisho.”

34. Maria akamjibu, “Yatawezekanaje hayo, hali mimi ni bikira?”

35. Malaika akamjibu, “Roho Mtakatifu atakushukia, na uwezo wake Mungu Mkuu utakujia kama kivuli; kwa sababu hiyo, mtoto atakayezaliwa ataitwa Mtakatifu, Mwana wa Mungu.

36. Ujue pia kwamba hata Elisabeti, jamaa yako, naye amepata mimba ingawa ni mzee, na sasa ni mwezi wa sita kwake yeye ambaye watu walimfahamu kuwa tasa.

37. Kwa maana hakuna jambo lisilowezekana kwa Mungu.”

38. Maria akasema, “Mimi ni mtumishi wa Bwana, nitendewe kama ulivyosema.” Kisha yule malaika akaenda zake.

Kusoma sura kamili Luka 1