Agano la Kale

Agano Jipya

2 Wakorintho 10:7-18 Biblia Habari Njema (BHN)

7. Nyinyi hutazama mambo kwa nje tu. Je, yupo mtu yeyote anayedhani kwamba yeye ni wa Kristo? Sawa! Basi, afikirie vilevile kwamba sisi pia ni wa Kristo kama yeye alivyo wa Kristo.

8. Hata kama nimezidi katika kujivuna kwangu juu ya ule uwezo aliotupa – uwezo wa kuwajenga na sio wa kubomoa – hata hivyo sijuti hata kidogo.

9. Sipendi mfikiri kwamba nataka kuwatisha nyinyi kwa barua zangu.

10. Mtu anaweza kusema: “Barua za Paulo ni kali na zenye maneno mazito, lakini yeye mwenyewe anapokuwa pamoja nasi ni mtu dhaifu, na hata anapoongea maneno yake ni kama si kitu.”

11. Mtu asemaye hivyo heri akumbuke kwamba hakuna tofauti ya yale tunayoandika katika barua wakati tuko mbali, na yale tutakayofanya wakati tutakapokuwa nanyi.

12. Kwa vyovyote hatungethubutu kujiweka au kujilinganisha na wale watu wanaojisifia wenyewe. Watu wenye kujifanya wao kuwa kipimo cha kujipimia, na watu wanaojilinganisha wenyewe kwa wenyewe, ni wapumbavu.

13. Lakini sisi hatutajivuna kupita kiasi; kujivuna huko kutabaki katika kile kipimo cha kazi aliyotukabidhi Mungu, kazi ambayo tunaifanya pia kwenu.

14. Hatukuruka mipaka tuliyowekewa wakati tulipokuja kwenu. Sisi tulikuwa wa kwanza kuja kwenu tukiwaleteeni Habari Njema juu ya Kristo.

15. Basi, hatujivunii kazi waliyofanya wengine zaidi ya kipimo tulichopewa; ila tunatumaini kwamba imani yenu itazidi miongoni mwenu kufuatana na kipimo alichotuwekea Mungu.

16. Hapo tutaweza kuihubiri Habari Njema katika nchi nyingine, mbali nanyi; na haitakuwa shauri la kujivunia kazi waliyofanya watu wengine mahali pengine.

17. Lakini kama yasemavyo Maandiko: “Mwenye kujivuna na ajivunie kazi ya Bwana.”

18. Anayekubaliwa si yule anayejisifu mwenyewe, bali yule anayesifiwa na Bwana.

Kusoma sura kamili 2 Wakorintho 10