Agano la Kale

Agano Jipya

2 Timotheo 4:1-10 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Nakuamuru mbele ya Mungu, na mbele ya Kristo Yesu atakayewahukumu watu walio hai na wafu, na kwa sababu anakuja kutawala akiwa Mfalme:

2. Hubiri huo ujumbe, sisitiza kuutangaza (iwe ni wakati wa kufaa au wakati usiofaa), karipia, onya na himiza watu ukiwafundisha kwa uvumilivu wote.

3. Utakuja wakati ambapo watu hawatasikiliza mafundisho ya kweli, ila watafuata tamaa zao wenyewe na kujikusanyia waalimu tele watakaowaambia mambo yale tu ambayo masikio yao yako tayari kusikia.

4. Watakataa kuusikia ukweli, watageukia hadithi za uongo.

5. Wewe, lakini, uwe macho katika kila hali; vumilia mateso, fanya kazi ya mhubiri wa Habari Njema, timiza kikamilifu utumishi wako.

6. Kwa upande wangu mimi, niko karibu kabisa kutolewa tambiko na wakati wa kufariki kwangu umefika.

7. Nimefanya bidii katika mashindano, nimemaliza safari yote na imani nimeitunza.

8. Na sasa imebakia tu kupewa tuzo la ushindi kwa maisha ya uadilifu, tuzo ambalo Bwana, Hakimu wa haki, atanipa mimi siku ile, na wala si mimi tu, ila na wale wote wanaotazamia kwa upendo kutokea kwake.

9. Fanya bidii kuja kwangu karibuni.

10. Dema ameupenda ulimwengu huu akaniacha na kwenda zake Thesalonike. Kreske amekwenda Galatia, na Tito amekwenda Dalmatia.

Kusoma sura kamili 2 Timotheo 4