Agano la Kale

Agano Jipya

1 Wakorintho 14:14-32 Biblia Habari Njema (BHN)

14. Maana, nikisali kwa lugha ngeni roho yangu ndiyo inayosali, lakini akili yangu hubaki bure.

15. Nifanye nini, basi? Nitasali kwa roho yangu, nitasali pia kwa akili yangu; nitaimba kwa roho yangu, nitaimba pia kwa akili yangu.

16. Ukimsifu Mungu kwa roho yako tu, atawezaje mtu wa kawaida aliye katika mkutano kuitikia sala yako ya shukrani kwa kusema: “Amina”, kama haelewi unachosema?

17. Sala yako ya shukrani yaweza kweli kuwa bora, lakini huyo mwingine haitamfaidia.

18. Namshukuru Mungu kwamba mimi nasema kwa lugha ngeni kuliko nyinyi nyote.

19. Lakini katika mikutano ya waumini napendelea zaidi kusema maneno matano yenye kueleweka ili niwafundishe wengine, kuliko kusema maneno elfu ya lugha ngeni.

20. Ndugu, msiwe kama watoto katika fikira zenu. Kuhusu uovu, muwe kama watoto wachanga, lakini katika kufikiri ni lazima muwe kama watu waliokomaa.

21. Imeandikwa katika sheria:“Bwana asema hivi:‘Kwa njia ya wenye kunena lugha ngeni,na kwa midomo ya wageni,nitasema na watu hawa,hata hivyo, hawatanisikiliza.’”

22. Hivyo basi, kipaji cha kusema lugha ngeni ni ishara, si kwa ajili ya watu wenye imani, bali kwa ajili ya wale wasioamini; lakini kipaji cha kutangaza ujumbe wa Mungu ni kwa ajili ya wale wanaoamini na si kwa ajili ya wasioamini.

23. Basi, kanisa lote linapokutana pamoja, na wote wakaanza kusema kwa lugha ngeni, kama wakija watu wa kawaida au wasioamini, je, hawatasema kwamba nyinyi mna wazimu?

24. Lakini, wote wakiwa wanautangaza ujumbe wa Mungu, akija mtu wa kawaida au asiyeamini, yote atakayosikia yatamhakikishia ubaya wake mwenyewe; yote atakayosikia yatamhukumu.

25. Siri za moyo wake zitafichuliwa, naye atapiga magoti na kumwabudu Mungu akisema: “Kweli Mungu yupo pamoja nanyi.”

26. Ndugu, tuseme nini, basi? Mnapokutana pamoja, mmoja aimbe wimbo, mwingine atoe mafundisho, mwingine awe na ufunuo kutoka kwa Mungu, mwingine atumie kipaji cha kusema kwa lugha ngeni na mwingine afafanue yanayosemwa. Yote yawe kwa ajili ya kulijenga kanisa.

27. Wakiwapo watu wenye vipaji vya kusema kwa lugha ngeni, waseme wawili au watatu, si zaidi, tena mmojammoja; na aweko mtu wa kufafanua yanayosemwa.

28. Lakini kama hakuna awezaye kufafanua, basi, mwenye kusema lugha ngeni anyamaze mkutanoni, aseme na nafsi yake mwenyewe na Mungu.

29. Kuhusu wale wenye kipaji cha kutangaza ujumbe wa Mungu, waseme wawili au watatu, na wengine wayapime maneno yao.

30. Ikiwa mmoja anaposema na mwingine wa wasikilizaji amepata ufunuo kutoka kwa Mungu, basi, yule anayesema anyamaze.

31. Maana nyote mwaweza kutangaza ujumbe wa Mungu, mmoja baada ya mwingine, ili nyote mpate kujifunza na kutiwa moyo.

32. Kipaji cha kutangaza ujumbe wa Mungu ni lazima kitawaliwe na huyo mwenye hicho kipaji.

Kusoma sura kamili 1 Wakorintho 14