Agano la Kale

Agano Jipya

1 Wakorintho 12:19-31 Biblia Habari Njema (BHN)

19. Kama sehemu zote zingekuwa kiungo kimoja, mwili ungekuwa wapi?

20. Ukweli ni kwamba, sehemu za mwili ni nyingi, lakini mwili ni mmoja.

21. Basi, jicho haliwezi kuuambia mkono: “Sikuhitaji wewe,” wala kichwa hakiwezi kuiambia miguu: “Siwahitaji nyinyi.”

22. Zaidi ya hayo, inaonekana kwamba sehemu zile za mwili zinazoonekana kuwa ni dhaifu ndizo zilizo muhimu zaidi.

23. Tena, viungo vile tunavyovifikiria kuwa havistahili heshima kubwa, ndivyo tunavyovitunza kwa uangalifu zaidi; viungo vya mwili ambavyo havionekani kuwa vizuri sana, huhifadhiwa zaidi,

24. ambapo viungo vingine havihitaji kushughulikiwa. Mungu mwenyewe ameuweka mwili katika mpango, akakipa heshima zaidi kiungo kile kilichopungukiwa heshima,

25. ili kusiweko na utengano katika mwili, bali viungo vyote vishughulikiane.

26. Kama kiungo kimoja kinaumia viungo vyote huumia pamoja nacho. Kiungo kimoja kikisifiwa viungo vingine vyote hufurahi pamoja nacho.

27. Basi, nyinyi nyote ni mwili wa Kristo; kila mmoja wenu ni kiungo cha mwili huo.

28. Mungu ameweka katika kanisa: Kwanza mitume, pili manabii, tatu waalimu; kisha ameweka wale wenye kipaji cha kufanya miujiza, kuponya na kusaidia; viongozi na wenye kusema lugha ngeni.

29. Je, wote ni mitume? Wote ni manabii? Wote ni waalimu? Wote ni wenye kipaji cha kufanya miujiza?

30. Je, wote ni wenye kipaji cha kuponya? Je, wote ni wenye kipaji cha kusema lugha ngeni? Je, wote hufafanua lugha?

31. Muwe basi, na tamaa ya kupata vipaji muhimu zaidi. Nami sasa nitawaonesheni njia bora zaidi kuliko hizi zote.

Kusoma sura kamili 1 Wakorintho 12